Katibu Mkuu Wizara ya
Viwanda na Biashara, Prof. Riziki Shemdoe, Leo tarehe 17 Julai, 2020 amekutana
na wazalishaji wa Saruji nchini kujadili changamoto ya bei na upatikanaji wake.
Katika kikao hicho
kilichofanyika katika ukumbi wa Eneo Huru la Uwekezaji kwa Mauzo Nje ya Nchi
(EPZA) Ubungo External jijini Dar es salaam, Katibu Mkuu alisikiliza maelezo ya
wazalishaji hao ambao walieleza changamoto mbalimbali zilizopelekea uhaba na
kupanda kwa bei ya Saruji Nchini.
Changamoto
zilizoelezwa na wazalishaji hao ni pamoja na Mvua kubwa iliyonyesha nchini
katika kipindi cha mwezi Machi, Aprili na Mei ambapo iliathiri zaidi uzalishaji
na usafirishaji wa Saruji, pili ni mlipuko wa Ugonjwa wa Korona (COVID 19)
ambapo asilimia kubwa ya vipuli vya mitambo vinaagizwa kutoka nje ya nchi, tatu ni
ujenzi wa miradi mbalimbali ya serikali inayoendelea nchini kama vile barabara
za kisasa, ujenzi wa reli ya kisasa ya mwendokasi, bwawa la kufua umeme la
Mwalimu Nyerere, ujenzi wa mji wa Serikali na Ikulu mpya ya kisasa jijini
Dodoma na ujenzi wa nyumba mpya za wakaazi jijini Dodoma.
Katika kikao hicho
Prof. Shemdoe amewashukuru wazalishaji wa Saruji kwa kuitikia wito wa Serikali
na kujadili hatma ya taifa lao hasa katika kuondoa kero ya kupanda kwa gharama
na pia upatikanaji wa Saruji.
Prof. Shemdoe amesema
kuwa kikao hiki kimetoa mwongozo mzuri wa muendelezo wa ushirikiano baina ya
wawekezaji na Serikali katika kutatua changamoto mbalimbali kwani kitendo cha
wenye Viwanda kuridhia kwa pamoja kuongeza uzalishaji kufikia kiwango
kilichokuwa awali pia kutokupandisha bei kitasaidia bei kushuka na Saruji
kupatikana kwa wingi ndani ya muda mfupi.
Wazalishaji hao wa
Saruji wamepongeza hatua hii iliyochukuliwa na Wizara ya Viwanda na Biashara kwani
imekuwa muhimili wa kuwaweka pamoja kuwasikiliza na kutatua changamoto
wanazokabiliana nazo. Wawekezaji hao wapo tayari kushirikiana na Serikali
katika kuboresha uchumi wa Nchi na Maisha ya Watanzania.