Search This Blog

Wednesday, January 22, 2020

ZIARA YA WAZIRI BASHUNGWA KIWANDA CHA KARATASI CHA MUFINDI


ZIARA YA WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA KATIKA KIWANDA CHA KARATASI CHA MUFINDI PAPER MILLS - IRINGA.
            Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Innocent Bashungwa amewapa wiki moja wawekezaji wa kiwanda cha karatasi cha Mufundi Paper Mills kilichopo eneo la Mgololo, kufika ofisini kwake Mkoani Dodoma kujieleza kuhusu uendeshwaji wa kiwanda hicho.
            Akizungumza katika ziara yake katika kiwanda hicho kilichopo mkoani Iringa, Mhe. Bashungwa ameshangazwa na jinsi wawekezaji hao walivyoshindwa kukiendeleza kiwanda hicho ambacho licha ya kuzalisha chini ya kiwango hakina malighafi ya kuzalisha karatasi nyeupe.
            Mhe. Bashungwa alisema kiwanda hakionyeshi kama kinaendana na dhumuni la kuanzishwa kwake hapa nchini.
            “Hayati Mwalimu Nyerere na Mhe. Rais John Pombe Magufuli sera zao zinafanana za kuendeleza viwanda nchini, lakini hapa sioni kama jambo hilo litafanikiwa” alisema Mhe. Bashungwa.
“Kiwanda hiki kilijengwa kwa gharama ya dola 260 milioni na kilipo binafsishwa kiliuzwa kwa dola 26 milioni kwa wawekezaji ikiwa ni pungufu ya asilimia 90 ya thamani yake ya awali”.
            Mhe.Bashungwa alisema fedha hizo dola 26 milioni hazikuingia Serikalini, bali  alipewa mwekezaji kwa lengo la kufanyia ukarabati kiwanda ili kiweze kufanya kazi kwa ufanisi zaidi.
            “Hadi sasa sijui kama hata kodi mnalipa kwa Serikali, natoa wiki moja nataka uje Dodoma kwa ajili ya kulizungumza suala hili”.
Mhe. Bashungwa aliongeza kusema kuwa kiwanda hiki kilitengezwa kwa ajili ya kuondoa tatizo la upatikanaji wa karatasi nchini.
            Aliongeza kuwa masuala ya usalama ya taifa yana sura tofauti tofauti na hata hili pia linaweza kuwa suala la usalama wa taifa iwapo mataifa mengine yakikataa kutuuzia karatasi kwa sababu moja au nyingine, itakuwa ni tatizo kubwa.
            “Watu watatushangaa tunashindwa kutengeza hata karatasi kwa ajili ya watoto wetu waliopo shuleni”.
            Kwa upande wake muwekezaji katika kiwanda hicho alisema kiwanda kinashindwa kuzalisha karatasi nyeupe kutokana na uhaba wa malighafi zinazozalisha bidhaa hiyo, hivyo alimuhaidi Mhe. Waziri kuzalisha karatasi hizo watakapopata utatuzi wa changamoto hiyo.
            Kiwanda hicho kinazalisha takribani tani 52,000 ambazo huuzwa ndani ya nchi na katika nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki.

MWISHO

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano Serikalini,
Wizara ya Viwanda na Biashara,
22 Januari, 2020.

Sunday, January 19, 2020

BRELA yakutana na kamati ya kudumu ya bunge ya viwanda, biashara na mazingira na kutoa taarifa ya majukumu yao.


BRELA YAKUTANA NA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA VIWANDA, BIASHARA NA MAZINGIRA NA KUTOA TAARIFA YA MAJUKUMU YAO

Wakala ya Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA) imetoa elimu ya Majukumu yao kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira katika ukumbi wa Bunge leo tarehe 18/01/2020.

Mafunzo hayo yaliandaliwa na Wizara ya Viwanda na Biashara kwa kushirikiana na BRELA. Lengo la mafunzo hayo ni kuwajengea uelewa kuhusiana na kazi na shughuli zinazofanywa na wakala katika kutoa huduma kwa jamii bila kusahau changamoto mbalimbali zinazoikabili BRELA ili kamati iweze kushauri.

Katika mawasilisho yaliyotolewa na Kaimu Mtendaji Mkuu wa Brela Bi. Roy Mhando alieleza shughuli mbalimbali zinazofanywa na wakala ambazo ni kusimamia Sheria ya Makampuni Sura ya 212, sheria ya majina ya biashara sura ya 213, sheria ya alama za biashara na huduma, Sheria ya Usajili wa Hataza, Sheria ya Leseni za Viwanda, Sheria ya Leseni za Biashara. Ameileza Kamati kuwa Wakala inafanya jitihada mbalimbali za kuhakikisha inatimiza majukumu yake kwa ufasaha na kuwafikia wateja wake kwa kutoa elimu kwa njia mbalimbali ikiwemo vyombo vya habari.

Makamu mwenyekiti wa kamati hiyo Mhe. Kanali mstaafu Masoud Ally Khamis (Mb) amempongeza Kaimu Afisa mtedaji Mkuu wa Wakala kwa kazi nzuri anayoifanya na kuitaka Wakala kuendelea kutoa Elimu ili wadau wa biashara wajue huduma mbalimbali wanazotoa hasa katika maeneo ya pembezoni ambapo wadau wa biashara hawajui umuhimu wa kurasimisha biashara zao pia hawana uelewa wa matumizi ya Tehama.

Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Innocent Lugha Bashungwa (Mb) amewashukuru Wajumbe wa Kamati ya kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kwa maoni na mawazo yao waliyoyatoa ambayo kwa kiasi kikubwa yamekuwa ya kuongeza ufanisi kiutendaji katika kuwahudumia wananchi pia ametoa maelekezo kwa BRELA kuwa waweke mkakati wa mawasiliano wenye lengo la kutangaza huduma zinazotolewa na Wakala kupita vyombo mbalimbali vya habari hasa kupitia redio za kijamii.

Mbunge wa Sumve Mhe. Richard Ndasa ameipongeza BRELA katika suala zima la kuwahudumia wateja kwani wamewawezesha wananchi wengi kupata huduma kwa urahisi kwani hivyo ndivyo inavyotakiwa katika kufikia uchumi wa kati wa viwanda ifikapo mwaka 2025.
Mbunge wa Ndanda Mhe. Cecil Mwambe amewashauri BRELA wawemakini kwenye kazi za kila siku ili kuondoa malalamiko na changamoto wanazopata wateja hii itasaidia kuongeza idadi ya wateja na pato la Taifa kwa ujumla.

Mbunge wa Viti Maalum Mhe. Hawa Mwaifunga ameiomba BRELA wafike katika wilaya na Mikoa mbalimbali hapa nchi kwani huko kuna wadau wengi wanaohitaji kujua faida za kurasimisha biashara zao.

Mbunge wa Monduri Julius Kalanga Laizer ameipongeza BRELA kwa kuandaa mfumo wao ambao wanaendelea kuuhuisha na akapendekeza ni vema taasisi zingine za biashara kuunganishwa pamoja.
Pia, amewapongeza watumishi wa BRELA kupitia kitengo cha TEHAMA wanaotoa msaada kwa wateja katika matumizi ya mtandao wa BRELA kwani wamekuwa wakisaidia sana wananchi pale wanapopata changamoto.
                      
Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Viwanda, Biashara na Mazingira Mhe. Kanali mstaafu Masoud Ally Khamis (Mb) alihitimisha kikao kwa kuwashukuru wajumbe wa kamati hiyo na kuwahimiza kuendelea kuishauri vema Serikali ili kuweza kufikia adhima ya Uchumi wa Kati unaongozwa na Viwanda ifikapo 2025.


Kaimu Meneja Mkuu wa wakala wa usajili na leseni BRELA Bi. Roy akieleza shughuli mbalimbali zinazofanywa na BRELA wakati wa semina elekezi iliyoandaliwa na BRELA kwa kamati ya kudumu ya bunge Viwanda na Biashara iliyofanyika bungeni, jijini Dodoma.

Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Innocent Bashungwa (Mb) akizungumza wakati wa semina ya elimu kwa wabunge wa kamati ya viwanda, biashara na mazingira.

Mbunge Mhe. Hawa Mwaifunga (katikati) akizungumza wakati wa semina ya kamati ya  Bunge Viwanda, Biashara na mazingira.

Ziara ya Naibu waziri Mhandisi Stella Manyanya (Mb) kiwanda kidogo cha kuchakata zabibu

ZIARA YA NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA KATIKA KIWANDA CHA KUCHAKATA ZABIBU CHA WENDECE, PIA KUZINDUA MASHINE YA KUCHAKATA ZABIBU ILIYOBUNIWA NA TEMDO KWA USHIRIKIANO WA SIDO DODOMA.


NAIBU Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Mhandisi STELLA MANYANYA (Mb), amesema kunahaja ya kuziwezesha kifedha taasisi za utafiti zinazobuni na kutekeleza teknolojia rahisi hapa nchini ili kufikia lengo la kuwa na viwanda na kufikia uchumi wa kati wa viwanda ifikapo mwaka 2025.

Naibu Waziri Manyanya ameyasema hayo jijini Dodoma wakati akizindua teknolojia mpya ya mashine ya kukamua mchuzi wa zao la zabibu katika kiwanda kidogo Cha WENDECHE kilichopo Kata ya Hombolo Bwawani, iliyobuniwa na TEMDO kwa kushirikiana na SIDO.

Alisema kuna haja ya kuziwezesha taasisi kama SIDO, TEMDO, CAMATEC, TIRDO na nyinginezo, kwani kwa muda mrefu taasisi hizo zilikuwepo lakini hazikuweza kunufaisha Watanzania. Lakini  tangu zimewezeshwa kifedha tayari matokeo yameanza kuonekana.
"Hii inafurahisha sana hizi taasisi zimewezsshwa na matokeo chanya tumeyaona, "alisema Manyanya.

Alisema kuwezeshwa kwa taasisi hizi pia kumesaidia  ukuaji wa viwanda nchini, na inatia moyo kuviwezesha zaidi..

Aidha amewahimiza Watanzania kuthamini vitu vinavyotengenezwa hapa nchini, ikiwamo kuthamini viwanda vidogo kwa sababu vinasaidia kutoa ajira kwa Watanzania, huku akiitaka SIDO kuhakikisha inasimamia wenye viwanda vidogo kuhakikisha wanapata mikopo kutoka benki ya kilimo Tanzania, TIDB, ili kuviongezea nguvu.

Alisema hakuna haja ya kubaki nyuma tunafanya kile tunachoweza na baadae kitaleta matokeo makubwa hapo baadae na kufikia Tanzania ya viwanda kama ilivyokusudiwa na Serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Mhe. Rais John P. Magufuli.

Alisema ni vema SIDO wakaweka jitihada ya kuwa karibu na watu hao ambao wakiwezeshwa wanaweza kuleta matokeo chanya katika kile ambacho wanafanya.

Mbali na hilo Naibu Waziri Manyanya amewapa wiki tatu TEMDO kuhakikisha wanawatengenezea mashine wajasiriamali ambao walitoa oda ya kutengenezewa mashine hiyo ili nao waendelee na shughuli ya uchakataji wa zabibu kwani mashine hizo ni nzuri na zina ufanisi wa hali ya juu.

Alisema hakuna sababu ya kuwacheleweshea kwa sababu wanahitaji kwa ajili ya kufanya maendeleo.

Kwa upande wake Meneja Taasisi ya ubunifu na uhandisi Mitambo, TEMDO, Mhandisi Alexander Komba, alisema kazi yao ni kubuni na kuendeleza Technolojia kwa ajili ya wajasiliamali wazalishaji, kisha kupeleka kwa SIDO ili ziweze kuwafikia walengwa. Kutokana na ushirikiano huo taasisi hizo mbili ambazo ziko chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara, waliweza kutatua changamoto ya kuchakata zao la Zabibu kwa haraka.
Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara Mhandisi Stellah Manyanya, akizungumza na wakulima wakati wa uzinduzi wa  Technolojia mpya ya mashine ya kukamua mchuzi wa Zao la Zabibu katika kiwanda kidogo Cha WENDECE kilichopo Kata ya Hombolo Bwawani, Wilaya ya Dodoma.




 Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara Mhandisi Stellah Manyanya,akikata utepe kuashiria uzinduzi wa  Technolojia mpya ya mashine ya kukamua mchuzi wa Zao la Zabibu katika kiwanda kidogo Cha WENDECE kilichopo Kata ya Hombolo Bwawani, Wilaya ya Dodoma.

Muonekano wa mashine ya kuchakata mchuzi wa Zabibu iliyobuniwa na kutengenezwa na TEMDO kwa ushirikiano wa SIDO.

Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara Mhandisi Stellah Manyanya,akiangalia waini zinazotengenezwa  katika kiwanda kidogo Cha WENDECE kilichopo Kata ya Hombolo Bwawani, Wilaya ya Dodoma.





Thursday, January 2, 2020

Mkesha wa kuukaribisha mwaka mpya 2020

Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Innocent Bashungwa akihutubia mamia ya wananchi waliojitokeza katika mkesha wa kuliombea taifa uliofanyika katika uwanja wa Uhuru jijini Dar es salaam, Tarehe 31 Desemba, 2019


MHE. INNOCENT BASHUNGWA AONGOZA MAMIA YA WATANZANIA KATIKA MKESHA WA KULIOMBEA TAIFA LA TANZANIA KATIKA KUUKARIBISHA MWAKA MPYA 2020.
Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Innocent Bashungwa ameongoza mamia ya watanzania katika mkesha wa kuliombea Taifa la Tanzania uliofanyika usiku wa Jumanne tarehe 31 Desemba, 2019 katika Uwanja wa Uhuru jijini Dar es salaam.
Katika mkesha huo wa kuukaribisha mwaka mpya 2020 uliohudhuriwa na viongozi mbalimbali wa serikali na wa dini ambapo waliongoza kwa dua na maombi kuliombea taifa letu, hasa viongozi waliobeba dhamana ya kuwatumikia watanzania ili waweze kutekeleza majukumu yao ipasavyo.
Akihutubia umati huo, Mhe. Bashungwa ambaye alimuwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli, alisema kwamba lengo la Serikali ya awamu ya tano ni kuhakikisha kuwa rasilimali za nchi zinatumika kunufaisha Watanzania. Katika kufanikisha hilo, Serikali inaendelea kujenga miundombinu wezeshi ikiwemo barabara, maji, umeme, huduma za afya, elimu n.k
Aidha Mhe. Bashungwa alisema kuwa azma ya Serikali ni kuhakikisha rasilimali za kilimo na utalii zinanufaisha wananchi walio wengi na sio wachache. Akitolea mfano kwenye sekta ya viwanda na biashara, maboresho yamefanyika BRELA, TBS na EPZA na kubainisha kuwa tayari fidia imekwishalipwa kwa ajili ya kujenga eneo maalumu la uchumi Kurasini litakalotumika kuchakata mazao ya kilimo na kutengeza ajira kwa kina mama na vijana ili kukuza uchumi wa nchi.
Katika mkesha huo Askofu Mkuu wa Tanzania Fellowship of Church (TFC) ndugu Godfrey Malasi alisema kuwa viongozi walioteuliwa na Mhe. Rais Magufuli, wana jukumu la kumsaidia huku wakiendana na kasi ya awamu ya tano na sio kumbebesha mzigo kwa kutotimiza wajibu wao kiutendaji.
Malasi alisema kuwa uelewa mdogo wa wananchi katika kusaidia kusukuma kasi ya uchumi wa viwanda imekuwa ni changamoto katika kuongeza kasi ya maendeleo kwani wamegeuka kuwa wachuuzi badala ya wazalishaji wa bidhaa hizo.
Alisema kuwa kauli mbiu ya Tanzania ya viwanda inamtaka kila mmoja kushiriki kikamilifu na siyo kuzurura mtaani ukiuza vifaa vya urembo badala ya kwenda kulima na kuzalisha mazao.
“Neno la Mungu linasema asiyefanya kazi na asile, ukimuona mtu ananing’iniza ushaga mwambie aende vijiji akalime tupate mazao sababu mambo ya kuning’iniza shanga haliwezi kuleta mabadiliko yoyote kwenye Tanzania ya viwanda,” alisema
Mkesha huo wa Kitaifa uliandaliwa na kuratibiwa na mashirika ya dini (Tanzania Fellowship of Churches) kwa Kushirikiana na Makanisa na huduma mbalimbali.
                                                                          
MWISHO
Imetolewa na:
Kitengo cha Habari na Mawasiliano,
Wizara ya Viwanda na Biashara,
31 Desemba, 2019

Prof. Kitila Mkumbo aanza kazi muda mchache mara baada ya kuapiswa kuwa Waziri wa Viwanda na Biashara

 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan akimuapisha Profesa Kitila Alexander Mkumbo kuwa Waziri wa Viwanda n...