![]() |
| Mhe. Innocent Bashungwa, Waziri wa Viwanda na Biashara akihutubia kwenye mkutano wake na wadau na wamiliki wa Viwanda vya nyama na ngozi nchini, kwenye ukumbi wa JNICC Jijini Dar es Salaam. |
Licha ya Tanzania
kushika nafasi ya pili kwa wingi wa mifugo barani Afrika, lakini bado nchi
hainufaiki na takwimu hizo kutokana na ubora mdogo wa mazao au bidhaa zitokanazo
na mifugo.
Mhe. Innocent Bashungwa,
Waziri wa Viwanda na Biashara amebainisha hayo leo wakati alipokutana na
kufanya kikao na wadau na wamiliki wa viwanda vya nyama na Ngozi nchini
Tanzania kwenye Kituo cha Mikutano cha Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam.
“Hadi sasa
Tanzania ina ng’ombe zaidi ya milioni 32, mbuzi zaidi ya milioni 20 na kondoo zaidi
ya milioni tano. Ili sekta hii iwe na tija kwenye uchumi wetu ni lazima uzalishaji
wa bidhaa za ngozi na nyama unapaswa kuongezeka kwenye viwanda vyetu vya ndani”
alibainisha kwenye hotuba yake ya ufunguzi.
Ili kukabiliana
na hali hii, Mhe. Bashungwa alisema kuwa tayari ameshaanza mazungumzo na nchi ambazo
zinaweza kutoa masoko makubwa ya bidhaa hizo, ambapo zitachangia kwa kiasi
kikubwa uzalishaji kuongezeka na pia kuongeza pato la taifa. Ajenda ya Serikali
ni kuhakikisha viwanda vinajengwa kwa wingi na kuweka mazingira sahihi ya
kulinda bidhaa za viwandani na kuhakikisha viwanda hivyo vinazalisha ili hatimaye
vilete faida kwa Tanzania na watu wake.
Kwenye mkutano huo,
Mhe. Bashungwa aliweka bayana mikakati ya Serikali kulinda bidhaa hizo kama
vile kutoza ushuru wa asilimia 80 ya thamani ya ngozi kuisafirisha nje ya nchi,
lakini bado viwanda vya ngozi vinazalisha asilimia arobaini tu ya uwezo wa
kuzalisha.
Kwa upande wa
wadau hao waliojitokeza kwa wingi, walisisitiza kuwa Serikali iendelee kuweka
mazingira wezeshi na kuweka nia ya dhati na kufanya maamuzi ya kufanya biashara.
Wazalishaji na wenye viwanda hawatafanikiwa iwapo Serikali haitaweka mkono
wake, ikiwemo kutochelewesha maamuzi muhimu.
“Kwetu sisi wadau
tunahitaji kuanza kuboresha mifugo yetu, kwasababu nyama nzuri yenye ubora,
inatokana na ng’ombe bora. Hata kama Tanzania ina mifugo mingi lakini
hatushindani kwenye soko kwasababu ng’ombe wetu sio bora kwenye export” alisema
Mzee Crisant Mzindakaya ambaye anamiliki mifugo na kiwanda.
Majadiliano ya
wadau na Serikali yametoa mwanga wa nini kifanyike ili sekta hiyo iwe na tija
zaidi kwa taifa ikiwemo kuongeza uzalishaji wa viwanda hivyo. Kati ya viwanda
vikubwa tisa vilivyopo nchini, viwanda vitano tu ndio vinavyofanya kazi ambapo
vinazalisha chini ya asilimia arobaini ya uwezo wao wa kuzalisha.
MWISHO
Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Viwanda na Biashara,
05 Desemba, 2019
![]() |
| Pichani juu na chini, washiriki wa mkutano huo wakiwemo taasisi mbalimbali za Serikali kama vile Hazina, Brela, Wizara ya Mifugo, Wizara ya Mambo ya Nje n.k. wakifuatilia mjadala wa mkutano huo. |




