![]() |
| Mhe. Bashungwa akiwa na Kiongozi wa Kiwanda cha Mwatex (wa pili kulia) wakati wa ziara yake kiwandani hapo, ambapo ameunda Tume ya Uchunguzi, kuhusu uendeshwaji wa kiwanda. |
Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Innocent
Bashungwa, amefanya ziara katika kiwanda cha Mwatex (2001) LTD kilichopo mkoani
Mwanza leo. Kiwanda hicho ambacho
kilibinafsishwa na Serikali na kupewa mwekezaji Amin Radhanin kimeajiri
wafanyakazi zaidi ya 600 na kinaendelea na uzalishaji kwa asilimia 60 kutokana
na changamoto mbalimbali.
Aidha katika ziara yake Mhe. Bashungwa alizungumza
na uongozi wa kiwanda na pia kusikiliza kero za wafanyakazi, ambapo wafanyakazi
walipata fursa ya kumueleza Waziri changamoto mbalimbali zinazowakabili.
Mtumishi wa kiwanda hicho aliyetambulika kwa jina
la Thomas Mashauri alieleza kuwa kuna rushwa katika masuala ya ajira, na kueleza
kwamba ili uweze kuajiriwa ni lazima utoe hongo ya kiasi cha shilingi elfu
hamsini (50,000) ndipo uajiriwe. Aidha aliongeza kusema kuwa wafanyakazi
wanalazimishwa kufanya kazi kwa kutumia mashine mbili kwa wakati mmoja pasipo
kuangalia jinsi gani mfanyakazi anaumia.
Ndugu Mashauri aliongeza kuwa wasimamizi katika
kiwanda hicho hawana kauli nzuri kwa wafanyakazi na pia wamekuwa wakali.
Pia wafanyakazi wa kiwanda cha MWATEX walieleza
changamoto ya upatikanaji wa vipuli (spare parts) vya mashine mbalimbali
katika kiwanda hicho inayopelekea mashine nyingingi kutokufanya kazi na
muda mwingi kutumika kwa ajili ya matengenezo.
Baada ya kusikiliza kero za wafanyakazi na kuona
utendaji wa kiwanda usioridhisha Mhe. Bashungwa ameagiza Wizara ya Viwanda na Biashara
kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, TIRDO, Dar Tech, VETA,
SIDO, NDC kuunda kamati maalumu ambayo itatembelea kiwanda hiki na kufanya
uchambuzi wa uendeshaji wa kiwanda kwa kushirikiana na msimamizi wa kiwanda.
Mhe. Bashungwa ametoa muda kuchunguza mwenendo wa
kiwanda hiki hadi kufikia tarehe 1/1/2020 kamati husika iwe imekamilisha kazi
na kukabidhi ripoti yake kwa Waziri.
Aidha Mhe. Bashungwa amesema kwamba ripoti husika itasaidia Serikali katika kutatua changamoto zinazokabili kiwanda hiki ili kiendelee kuzalisha kwa asilimia 100 kama ilivyo mkakati wa Serikali ya Awamu ya Tano wa kuhakikisha viwanda vyote vilivyobinafsishwa vinafufuliwa, vinafanya kazi na kuongeza uzalishaji kwa asilimia 100, ili kutengeneza mnyororo wa thamani ya mazao.
MWISHO
Imetolewa
na:
Kitengo
cha Habari na Mawasiliano,
Wizara
ya Viwanda na Biashara,
11
Desemba, 2019







